Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo leo Oktoba 22, 2021 imeishinda timu ya wanawake ya Wizara ya Nishati kwa kuwafunga magoli 23:21 kwenye Mashindano ya Michezo ya Wizara na Idara za Serikali Tanzania (SHIMIWI) yanayoendelea mjini Morogoro.
Akizungumzia ushindi huo, Mwalimu Alice Choaji amesema ushindi walioupata leo umekuwa ni mwanzo mpya na hamasa kwao kuendelea kufanya maandalizi mazuri tayari kwa michezo inayofuata.
“Wachezaji wapo vizuri, wanaendelea kujituma kwa ajili ya Ofisi yao na kujenga afya za miili yao na wamehamasika vizuri, tunaamini kwa ushirikiano mzuri tunaopata kutoka kwa viongozi wetu hatutawaangusha kazi ndiyo imeanza” alisema Mwl. Alice.
Kwa upande wake Nahodha wa Timu Jane Thawe lengo lao ni kufikia hatua ya robo fainali na hatimaye hatua zinazofuata za kuelekea ubingwa na amewahamasisha wachezaji wenzake kuendelea kufanya mazoezi kwa juhudi na maarifa zaidi hatua itakayowasaidia kufikia ubingwa wa michuano hiyo ambao wanautamani kuupata.
Aidha, timu ya wanawake ya Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo imewashinda watumishi wenzao wa umma kutoka Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Kilimanjaro (RAS) kwa ushindi wa kuwavuta mara mbili (2:0) hatua inayowapa hamasa ya kuendelea vizuri katika michuano hiyo inayoendelea mjini Morogoro.
Kwa mujibu wa Kanuni za mchezo wa kuvuta kamba Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo ilimaliza mchezo huo kwa mivuto miwili na hivyo kuibuka kidedea hatua iliyopelekea kumaliza mchezo mapema na kuondokana na ulazima wa kuwa na mivuto mitatu endapo wapinzani wao wangefanikiwa kuwavuta hata mara moja.
Mashindano ya SHIMIWI yanashirikisha Mchezo wa mpira wa miguu, Mchezo wa Netiboli, Mchezo wa Bao, Kuvuta Kamba, Mchezo wa Drafti, Mchezo wa Karata, Kufukuza Kuku, Riadha pamoja na mchezo wa Magunia.
Nahodha wa timu ya mchezo wa netiboli ya Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo Jane Thawe (aliyechezea nafasi ya GA) akiongoza timu ya Wizara yake dhidi ya Wizara ya Nishati ambao walifungwa kwa jumla ya magoli 23:21 kwenye Mashindano ya Michezo ya Wizara na Idara za Serikali Tanzania (SHIMIWI) yanayoendelea mjini Morogoro.
0 Comments