Header Ads Widget

WAZIRI SIMBACHAWENE AWAONYA WANAOHAMASISHA UVUNJIFU WA AMANI NCHINI

 

Na Hamida Ramadhan,Matukio Daima Media Dodoma 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene amewaonya wale wote wanaohamasisha uvunjifu wa amani nchini huku akiwasihi Wanawake wasijiingize kwenye  mtego huo kwani madhara yake ni makubwa.



Mhe.Simbachawene ametoa kauli hiyo leo wakati akifungua Kongamano la 16 la Wanawake Waombolezao Kitaifa waliokusanyika jijini Dodoma kwa ajili ya kuombea amani ya nchi ya Tanzania  hususan katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi  Oktoba mwaka huu. 


Amesema maendeleo yaliyopo nchini ikiwemo huduma za kijamii ni matokeo ya amani na utulivu uliopo, "Hatuwezi kubomoa ili tujenge upya, ni lazima tukumbatie majadiliano kama Taifa hatuwezi tukawa tunafikiria sawa ni lazima tutofautiane" amesisitiza Mhe.  Simbachawene.

"Kuna watu wanasema Tanzania hii hakuna amani  wala maendeleo yaliyofanyika tangu tupate uhuru, hivyo tuandamane,  hapo ndipo tutapata haki yetu, wananchi kataeni huo ushetani"  amesema Waziri Simbachawene 


Kufuatia hatua hiyo Mhe.Simbachawene amewataka Watanzania  kuwapuuza wale wote wenye maslahi binafsi wanaotaka kuwaona  wananchi wanachukiana wenyewe kwa wenyewe  na hatimaye kuanza  kuuana wao kwa wao  kwa chuki za kupandikizwa. 


Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Tanzania  Fellowship of Churches, Godfrey Malasi amesema Kongamano hilo ni mahsusi kwa ajili ya  maombi maalum ambayo yamekuwa yakifanyika kila mwisho wa mwaka  kwa lengo la kuliombea amani  Taifa la Tanzania na kuwahimiza Watanzania kumjua na kumtumikia Mungu.



Sisi tunavyofurahia amani na utulivu tuliyonayo, wenzetu huko kwingine wanalia na kusaga meno, hivyo tuna wajibu wa kuzidi kumuomba Mungu atupe hekima ili tuzidi kuilinda amani yetu, amesisitiza Askofu Malasi.


 Vita sio nzuri kabisa,  sisi tumepewa uwezo wa kupigana vita vya rohoni ili kuzuia vita vinavyoonekana "  amesema 

Aidha, Askofu Malasi amesema Kongamano hilo limekuwa likiombea maadili mema ya Taifa hususan katika kipindi hiki ambacho vijana wameathiriwa na vitendo vya ushoga, usagaji na utoaji mimba, vitendo ambavyo vinakwenda  kinyume na tamaduni zetu.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI