JAMII imeshauriwa kujikita katika kilimo cha mkonge ili kiweze kuwanufaisha kiuchumi.
Wito huo umetolewa Julai 10 mwaka huu Jijini Dar es Salaam na Mkuu wa sehemu ya masoko wa Bodi ya Mkonge Tanzania "Tanzania Sisal Board"- (TSB), David Maghali, katika maonyesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba yanayoendelea Dar Es Salaam.
Amesema zao la mkonge lina faida kubwa kutokana na kuzalisha bidhaa nyingi kwa uchumi wa mkulima taifa kwa ujumla hivyo wananchi hawana budi kukichangamkia.
"Mkonge una faida kubwa kuanzia mbegu hadi mabaki yake na tuna soko la uhakika istoshe nchi yetu imejaliwa kuwa na ardhi yenye rutuba. Wananchi wachangamkie fursa ili kujikwamua," alisema Maghali.
Naye Afisa Kilimo Mwandamizi wa bodi hiyo Emmanuel Lutego ametaja faida za mabaki ya mkonge kuwa ni nishati safi ya kupikia.
”Mbali na nyuzi kwenye mabaki ya mkonge tunapata mbolea inayotumika kwenye mashamba ya mkonge na mengine, mabaki yake hutupatia uyoga, chakula cha mifugo kwa kulishia ngombe, kuku na mifugo mingine
“Kupitia mabaki hayo tunaweza kuzalisha nzi chuma(back soldiers flies) ambao katika hatua ya ukuaji tunapata lava ambao watatumika kama chakula mbadala badala ya dagaa kwa ajili ya kunenepeshea au kulishia mifugo ambacho kina protini ya kutosha,” amesema Lutego.
Ameongeza pia katika mabaki hayo huzalisha bio gesi nishati safi kwa ajili ya kupikia. ” Kama tunavyofahamu Rais Samia Suluhu Hassan ni Championi katika nishati safi kwahiyo mkonge nao mojawapo ya bidhaa ambayo tunapata kwenye zao hilo ni gesi ambayo itatumika kupikia na kuendeshea mitambo, mmea wa mkonge huweza kutengenezewa pombe aina ya tikila(spiriti) pamoja na bidhaa ya asali.’ amesema Lutego.
Amesema Tanzania ina sifa duniani kwa kuzalisha mkonge bora hivyo wamejiwekea lengo la kulinda heshima ya nchi kwa kuleta mashine kubwa nzuri za kuchakata zitakazoongeza uzalishaji ili kupata mkonge ulio bora zaidi.
Amesema wamejiwekea lengo la kufikisha tani 120,000 za uzalishaji wa zao hilo na hayo yatawezekana ikiwa mashine za uchakataji zitaongezeka.
0 Comments