Na Hamida Ramdhan, MatukioDaima APP Dodoma
MAMLAKA ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imetumia maonesho yanayoendelea jijini Dodoma kuwaelimisha wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na fursa lukuki zinazopatikana katika sekta ya mafuta na gesi asilia, hasa mkondo wa juu wa petroli.
Akizungumza katika banda la PURA kwenye maonesho hayo, Mkuu wa Kitengo cha Ushirikishwaji wa Wazawa na Ushirikiano wa Ndani, Bw. Charles Nyangi, alisema kuwa PURA ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Petroli ya mwaka 2015, ikiwa na jukumu la kusimamia na kudhibiti shughuli zote za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia nchini.
“Moja ya majukumu yetu muhimu ni kuhamasisha ushiriki wa wazawa kwenye shughuli za mkondo wa juu wa petroli. Ushiriki huu umegawanywa katika maeneo matatu makuu: kupitia ajira, kupitia ujasiriamali kwa maana ya utoaji wa bidhaa na huduma, na kupitia uwekezaji,” alieleza Nyangi.
Ameongeza kuwa kushiriki kwa PURA katika maonesho hayo kunalenga kuwaelimisha wananchi juu ya majukumu ya mamlaka na namna wanavyoweza kushiriki kikamilifu katika sekta hiyo muhimu ya kiuchumi.
Aidha, Nyangi alieleza kuwa gesi asilia imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa, hasa kwenye sekta ya uzalishaji wa umeme, na akatoa mfano wa uwekezaji wa Serikali katika miradi ya umeme wa bwawa ambayo inachangia kuongeza upatikanaji wa nishati endelevu.
“Gesi hii ni muhimu kwa matumizi ya majumbani, viwandani, na sasa tunasonga mbele kuhakikisha inatumika pia kwenye magari. Tayari gesi inapatikana Mtwara, Lindi na Dar es Salaam, lakini Serikali inaendelea kuwekeza ili kusambaza huduma hiyo katika mikoa mingine,” alibainisha.
Kupitia usimamizi wa PURA, Serikali inalenga kuhakikisha kuwa rasilimali za mafuta na gesi asilia zinawanufaisha Watanzania wote kwa kuimarisha ushirikishwaji wa wazawa, kukuza ujuzi wa kitaifa na kuongeza fursa za kiuchumi.
0 Comments