SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ipo katika mchakato wa kuunda kamati maalumu ya kutafuta fedha kuongeza fedha za ufadhili kwa ajili ya wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi, uhandisi na elimu tiba nje ya nchi.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda wakati akizindua bweni la wasichana, vyumba vya madarasa na maabara sekondari ya Kizimkazi Dimbani ambavyo vimejengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).
Amesema serikali inaendelea kuhamasisha wanafunzi wengi wajitokeze kusoma masomo hayo kwani hakuna taifa linaweza kuendelea kama halina. wataalamu katika sekta hizo.
Ameeleza tayari serikali imeanzisha mfuko maalumu wa Samia Scolaship ambapo mwanafunzi katika maeneo hayo anapata ufadhili na serikali kwa asilimia 100 na kugharamiwa kila kitu anapkwenda nje kusoma.
“Tumeshatenga fedha lakini tunataka kuunda kamati maalumu ya kutafuta fedha kwa kushirkiana na mabenki ili kuongeza mfuko huo kuwasaidia wanafunzi kusoma,” amesema
Ametumia fursa hiyo kuwataka walimu, wazazi kuwahimiza wanafunzi kusoma masomo hayo kuanzia kidato cha kwanza ili wanufaike na fursa hiyo.
Kwa mujibu wa Profesa Mkenda amesema wakati wanaanzisha ofisi ya Atomu Zanzibar walitafuta watu wenye sifa lakini wamebaini kuna chngamoto kubwa ya watu wenye elimu hiyo hivyo wameanza mpango kuwekeza katika eneo hilo kuwasomesha watu wenye sekta hiyo.
Amesema wameagiza sasa itengwe bajeti katika taasisi hiyo kwa ajili ya kusomesha wataalamu hao.
Mkurugenzi Mkuu wa Tasaf Shadrack Mzirai amesema katika kipindi cha pili cha uhaulishaji wa fedha kwa kaya masikini jumla ya Sh48.84 bilioni zimetolewa kwa kaya 53,441.
Amesema zaidi ya miradi 761 yenye thamani ya Sh15 bilioni imeibuliwa kati ya kiasi hicho, Sh1.98 bilioni zimetumika kununua vifaa huku Sh13 bilioni zikitumika kulipa ujira kwa wananchi wanaoshiriki kujenga miradi hiyo ambao wanatokana na kaya hizo zinazonufaika na mfuko.
“Katika miradi iliyoibuliwa ni pamoja na barabara, ujenzi wa shule, mazingira uvuvi na miundombinu hivyo wananchi hao kujiongezea kipato kile kinachotokana na mfuko wenyewe.
Amesema kupitia mpango huo wamenzisha vikundi vya ujasiriamali mbapo zidi ya wananchi 23, 000 wamenufaika.
Amesema Tasaf imeunganisha kanzi data Bodi ya Mikopo kuwasaidia wanufaika wa Tasaf ambapo wengi wameendelea kunufaika.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Khamis Abdalla Said amesema vyumba vinne vya madarasa vyenye uwezo wa kubeba wanafunzi 180 sawa na wastani wa wanafunzi 45 kila darasa.
Kwa mujibu wa katibu Mkuu maabara na vyumba hivyo vimegharimu zaidi ya Sh400 milioni.
Amesema Serikali inaendelea kuhakikisha inaondoa changamoto za elimu na wanafunzi wasisome mikondo miwili.
0 Comments