Na Hamida Ramadhan Matukio Daima app Dodoma
KUTOKA na Mvua zinazoendelea kunyesha za El Nino ambazo hadi sasa bado zinaendelea katika baadhi ya maeneo nchini Moja ya athari za mvua hizo ni uharibifu wa miundombinu,
ikiwemo barabara za kwenye hifadhi za taifa zilizo chini ya Shirika la Hifadhi za
Taifa (TANAPA) ikiwemo Serengeti.
Hayo yamesemwa leo jijini hapa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) na Msemaji Mkuu wa Serikali
Mobhare Matinyi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema Kwa eneo la kaskazini mwa nchi ambako ndiko Serengeti ilipo, El Nino ilikuja wakati wa majira ya mvua za vuli za Oktoba hadi Desemba na kisha kuendelea kunyesha na kuunganisha na majira ya mvua za masika ya Machi hadi Mei.
Amesema Kwa mujibu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ingawa
chanzo cha El Nino, ambacho ni ongezeko la joto katika bahari ya Pasifiki bado kipo lakini sasa kinaendelea kupungua.
Hata hivyo, amesema kwa kuzingatia kuwa kuna visababishi na viashiria vingine vya mvua kubwa, bado mvua hizi zitakuwa ni za wastani au zaidi, ikimaanisha mvua zitakuwa kubwa kuliko ilivyozoeleka.
Amesema Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ambayo pia imeathirika na El Nino, ni hifadhi ya pili kwa ukubwa nchini yenye kilomita za mraba 14,763.
Ameeleza kuwa Hifadhi kubwa zaidi
nchini ni Ruaha yenye kilomita za mraba 19,822 lakini Serengeti ndiyo hifadhi
ya kwanza nchini kwa kuingiza watalii wengi zaidi.
Hivyo basi, kwa kuangalia hatua za muda mrefu, TANAPA inatafuta njia mbadala za kuzitunza barabara hizi, Njia hizo mbadala ni zile za kuweka tabaka gumu kama la zege au lami.
Amesema Kwa kuzingatia kanuni za uhifadhi, TANAPA na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinaandaa andiko la kitaalam la kuwasilisha kwenye Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)
kuhusiana na suala la kuweka tabaka gumu kwani Serengeti imo katika Orodha ya Urithi wa Dunia inayosimamiwa na Kamati ya Urithi wa Dunia ya UNESCO.
Amebainisha kuwa, Njia ya kutumia andiko la kitaalam ndiyo iliyotumiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya
Eneo la Ngorongoro (NCAA) ambapo sasa imepata kibali cha kujenga barabara yenye tabaka gumu.
Amesema Barabara hiyo ndiyo pia inayoingia hifadhini Serengeti kwa
kuzingatia kuwa vivutio hivi viwili maarufu duniani vinapakana.
Amesema Kuna barabara kuu nne zenye changamoto zaidi kutokana na upitaji wa magari makubwa ya abiria na mizigo yanayokwenda mikoa ya jirani ya Mara, Arusha, Manyara, Mwanza, Shinyanga na Simiyu ambazo TANAPA ndizo inazozilenga katika mkakati wake wa mbinu mbadala ya tabaka gumu iwapo itakubalika.
"Barabara hizo pia hupitisha magari ya watalii kati ya 600 hadi 800 kwa siku;
hivyo kuharibika mara kwa mara hata kama hakuna mvua kubwa. Barabara hizo zenye jumla ya kilomita 291 tu (asilimia 9) kati ya kilomita 3,176 za mtandao wa barabara katika hifadhi nzima ni kama ifuatavyo:
Ø Golini – Naabi - Seronera (km 68)
Ø Seronera – Lango la Ndabaka (km 121)Ø Seronera – Lango la Ikoma (km 30)Ø Banagi (Seronera) – Lobo – Lango la Kleins (km 72), " Amesema Msemaji huyo
Amesema TANAPA inatarajia kwamba utatuzi wa kudumu utapatikana katika barabara kuu zinazoihudumia Serengeti na hivyo kuongeza idadi ya watalii nchini kwa kiasi
Ameeleza kuwa Hadi sasa, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti imeshinda Tuzo ya Hifadhi Bora Afrika kwa miaka mitano mfululizo.
"Serengeti ni maarufu zaidi kwa tukio la uhamaji wa wanyama aina ya nyumbu ambapo kila mwaka nyumbu wapatao milioni 1.5 hutumia miezi kumi wakizunguka ndani ya hifadhi ya Serengeti na kisha kwenda
nchi jirani na kurejea, " Amesema Msemaji huyo.
Amesema Katika uhamaji huo tukio la kusisimua zaidi ambalo ndilo huvuta watalii wengi ni lile la kuvuka mto Mara pamoja na matawi yake.
Aidha amesema Serengeti ambayo ilianzishwa mwaka 1959, ni kati ya hifadhi chache Afrika na
duniani ambapo mtalii anaweza kuona wanyama wote watano maarufu, yaani
simba, chui, tembo, nyati na kifaru. Wanyama wengine wengi hifadhini Serengeti ni pamoja na pundamilia, twiga, jamii ya swala, duma, viboko na mamba.
TANAPA inasimamia na kuendeleza jumla ya hifadhi 21 zenye ukubwa wa
kilomita za mraba 98,908.88 - sawa na asilimia 10.2 ya eneo zima ya Tanzania.
Hifadhi hizo ni: Arusha (Arusha), Burigi-Chato (Geita na Kagera), Gombe (Kigoma), Ibanda-Kyerwa
(Kagera), Katavi (Katavi), Kilimanjaro (Kilimanjaro), Kitulo (Njombe na Mbeya), Mahale (Katavi na
Kigoma), Manyara (Arusha na Manyara), Mikumi (Morogoro), Mkomazi (Kilimanjaro na Tanga),
Ruaha (Iringa, Dodoma na Mbeya), Kisiwa cha Rubondo (Geita na Kagera), Rumanyika-Karagwe
(Kagera), Saadani (Pwani na Tanga), Kisiwa cha Saanane (Mwanza), Serengeti (Mara, Arusha na
Simiyu), Tarangire (Dodoma na Manyara), Milima ya Udzungwa (Morogoro na Iringa), Mto Ugalla
(Tabora na Katavi) na Nyerere (Pwani, Morogoro na Mtwara).
Amesema TANAPA ina jukumu la kuendelea kuhifadhi wanyamapori, bioanuai na makazi ya wanyama katika hifadhi za taifa kwa ajili ya vizazi vijavyo; na pia kuongeza idadi ya watalii na mapato yatokanayo na utalii katika hifadhi zote za taifa.
"Katika kutekeleza majukumu haya kwa ufanisi, TANAPA imefanikiwa kutoa
mchango mkubwa katika idadi ya watalii ambapo kwa mwaka 2022 ilichangia
watalii 697,264 kati ya 1,454,920 walioingia nchini, " Amesema .
Na kuongeza "Kwa mujibu wa takwimu za Baraza la Utalii la Dunia (World Travel and Tourism
Council – WTTC) kwenye ripoti ya Tanzania ya mwezi Februari 2023, asilimia 90.7 ya wageni wanaoingia nchini hutembelea vivutio vya hifadhi za taifa, hifadhi ya Ngorongoro na fukwe za Zanzibar, " Amesema .
ONGEZEKO LA WATALII KATIKA HIFADHI YA SERENGETI
Kufuatia mafanikio makubwa ya filamu ya Royal Tour – ambayo Mhe. Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, yeye mwenyewe
alikuwa mshiriki mkuu, idadi ya watalii wanaokuja Serengeti sasa imekwenda
juu kupita malengo makubwa yaliyowekwa kwa mwaka huu wa fedha.
Taarifa ya mafanikio hayo ni kwamba, ingawa makadirio ya idadi ya watalii kwa mwaka 2023/24 yalikuwa 1,387,987 lakini mpaka kufikia Februari 2024 (miezi nane tu kuanzia Julai 2023), jumla ya watalii 1,451,176 wameshaingia.
MIUNDOMBINU YA SERENGETI
Hifadhi za taifa 21 zilizo chini ya TANAPA zina barabara zenye urefu wa jumla ya kilomita 16,470.6 ambapo Serengeti peke yake ina jumla ya kilomita 3,176. Kimsingi ndiyo hifadhi yenye mtandao mrefu zaidi wa barabara ambazo ni za udongo ama changarawe. Barabara hizi zimegawanyika katika barabara kuu zilizo chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini Tanzania (TARURA) na kundi la pili la barabara ndogondogo zilizo chini ya TANAPA yenyewe.
Serengeti pia ina viwanja vidogo vya ndege (airstrips) vipatavyo saba ambavyo ni Serengeti, Kogatende, Lobo, Lamai, Grumeti, Kusini na Fort Ikoma.
Hivyo basi, watalii wanaokuja Serengeti huja ama kwa njia ya barabara au ndege
ndogo kutoka maeneo mbalimbali nchini yanayopokea wageni kutoka nje au
kutoka kwenye vivutio vingine kama fukwe.
"TANAPA yenyewe ndiyo huzitunza barabara hizi na viwanja vya ndege ili
kuhakikisha kwamba watalii wanaendelea kuingia hifadhini, " Amesema Msemaji huyo
Amebainisha kuwa TANAPA hutumia wataalam wake pamoja na vifaa vyake. Na kwa mujibu wa sera yake ya uhifadhi, TANAPA hutumia changarawe kutoka ndani ya hifadhi kwa ajili ya matumizi endelevu, kupunguza gharama na kuepuka kuingiza mimea-vamizi ambayo huharibu malisho ya wanyama na pia kuleta magonjwa ya mimea.
Katika mtandao wa kilomita 3,176 za barabara za Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, kilomita 2,407 ni za udongo na kilomita 769 ni za changarawe. Kutokana na hojakadha wa kadha za kiuhifadhi hakuna barabara za lami wala zege.
Maji yanayotumika katika matengenezo ya barabara hizi hutoka kwenye visima
badala ya mabwawa na mito iliyopo hifadhini ili kuwaachia wanyama maji hayo ambayo ni muhimu kwa uhai.
Pale ilipotokea changamoto ya mvua za El Nino kulitokea mafuriko makubwa
hifadhini kiasi cha kufunika barabara kuu zinazoleta watalii. Uharibu ulikuwa
mkubwa.
Hivyo basi, TANAPA ilichukua hatua za haraka za awali za kuzifanyia
matengenezo barabara hizo ili kuhakikisha kwamba wageni wanaendelea kutalii
na usafirishaji haukwami.
Mwisho
0 Comments