Header Ads Widget

MADEREVA 257 WALIORUDI DARASANI VETA IRINGA WAFANYA VIZURI MTIHANI WA VITENDO


NA MATUKIO DAIMA APP 

JUMLA  ya  madereva  257   wa  mabasi ya  abiria  na  malori  ya  mizigo  kutoka  mkoa  wa  Iringa  na nje ya  mkoa  huo waliokuwa  wamerudi  darasani  kujifunza  upya mafunzo ya  udereva  katika  chuo  cha  ufundi  stadi (VETA)  Iringa  wamefaulu mtihani wa  vitendo katika  chuo   hicho .


Mratibu  wa mafunzo hayo  Edmund Enugu  akizungumza  Leo   wakati  wa  mtihani  wa mwisho  wa  darasani kwa madereva  hao chuoni   hapo alisema  kuwa  jumla ya  madereva  wa mabasi ya  abiria 215  na  madereva  42  wa  malori  akiwemo  mwanamke  mmoja  walijiunga na mafunzo ya  muda  mfupi  chuoni  hapo  kufuatia   agizo la  serikali la  kutaka  madereva  wote  ambao  hawana vyeti  kurudi vyuo  kusoma .



Alisema  kuwa   mafunzo hayo  yalikuwa ni  ya   wiki  mbili na kuwa baada ya mafunzo hayo  wamefanya  mtihani  wa  vitendo chini ya askari wa  usalama  barabarani  kwa  kujaribiwa  uwezo wao  wa  udereva  na  wote  wamefaulu  mtihani  huo  wa  kwanza na jana  wameingia katika  mtihani  wa  pili  wa  darasani  ambao wanafunzi  wote  wamefanya  mtihani  huo  .


Msajili  wa  chuo  cha  VETA   Baltazar Kinyamaganga  alisema  serikali  imeamua  kulifanya  Taifa  kuwa ni Taifa la  viwanda  hivyo  jukumu  la  kuandaa mafundi  ni la VETA na  ofisi yake ya  msajili  ni usimamizi  wa  vyuo  vya  VETA  na   kuwa vyuo  vya  VETA  Iringa  vinaendelea kutekeleza malego ya  serikali  ya  kuona   vijana  wanakuwa na  ujuzi  wa  ufundi  mbali  mbali  kupitia  kozi  fupi na  ndefu  .


Kuwa  kozi  fupi ni  kuanzia  wiki  mmoja  hadi  wiki  sita  na  mafunzo ya  muda  mrefu ni  kuanzia mwezi  mmoja  hadi  miezi  sita  na kuwa kupitia  mafunzo  hayo  mwamko wa  jamii  kupata  mafunzo  VETA  umekuwa mkubwa   zaidi .



Alisema  serikali  ya  awamu ya  sita   chini ya  Rais  Dkt  Samia Suluhu  Hassan imeendelea  kutoa fedha  kwa  ajili ya  ujenzi  wa  vyuo  vya  VETA  katika kanda  ya  nyanda  za  juu  kusini na tayari  vyuo  katika  wilaya ya  Iringa na Wanging'ombe unakwenda  vizuri  wakati Ludewa  umekamilika  na  wilaya ya  Kilolo  pesa  tayari  imetolewa .


Kinyamaganga  alisema  kanda  ya  Iringa  mbali ya  chuo cha  VETA  Iringa  kinachofanya  kazi  vizuri  pia  kuna  vyuo  vya Songea, Namtumbo ,Makete  na  Nyasa  navyo  vinaendelea  vema.


Hivyo  aliwataka  wahitimu katika  mafunzo  mbali mbali  ndani ya  vyuo  vya  VETA  hasa  madereva  ambao  wanatoka  nje ya  nchini  kuendelea   kuwa  wazalendo la Taifa  kwa  kueneza  sifa  nzuri ya  nchini  badala ya  kuanikia  siri ama  kulitangaza  Taifa  vibaya  nje .


Pia  kuepuka  kujihusisha na  sifa  mbaya  za  wizi na  kusafirisha mali  za magendo kwani  ni  sifa  mbaya  ambazo zinalichafua  Taifa na  kuharibu  taswira  nzima ya kazi ya   udereva.



Washiriki  wa  mafunzo  hayo Yowel  Chatanda na Richard  Chongole walisema  kuwa  mafunzo hayo  kwao  ni  msaada  mkubwa kwani  kabla ya  mafunzo  walikuwa  wakifanya kazi ya  udereva  pasipo  kuingia  darasani na  siku  zote  walijikuta wanapigwa  faini  za  uzembe  barabarani  kutokana na kutojua  sheria  za  usalama  barabarani ambazo  sasa  wamepatiwa .



Chongolo  alisema   kuna  wakati  alipigwa  faini na askari  wa  usalama  barabarni  baada  ya  kushindwa  kujua kosa lake na  hivyo kutakiwa  kulipa  faini  kwa  kutojua kosa  lake.


"  Nilisimamishwa na  askari wa usalama  barabarani  aliniuliza  unajua kosa  lako  nikasema  sijui kosa  akaniambia kutojua kosa  pia  ni  kosa   hivyo  natakiwa  kulipa  faini  kwa  kosa la  kutojua kosa na  nililazimika  kulipa  faini kwa  kutojua kosa" alisema



Mkuu  wa  chuo  cha  VETA  Iringa  Pasiens  Nyoni   alisema  kuwa  chuo  hicho  kimeendelea  kutoa  mafunzo  ya  udereva  na mafunzo  mengine  mbali  mbali  kwa  ajili ya  kuwaandaa  vijana  kwenda  kujitegemea na kuongeza  ajira    katika  fani  za  ufundi  .


Alisema  kuwa   pamoja na  VETA  kuendelea  kutoa  mafunzo  ya udereva  ila  bado  ajali  zinaendelea  kutokea  na ndio  sababu ya kuja na mafunzo ya  muda  mfupi  kwa madereva  kama  sehemu ya  kuwakumbusha mafunzo  waliyoyapata  darasani  na kupitia mafunzo hayo  madereva  wameendelea  kukumbuka  sheria mbali  mbali  za  usalama  barabarani.


Nyoni  alisema  kuwa  kupitia mafunzo hayo ya  muda  mfupi  madereva  wameendelea  kukumbushwa  sheria  mbali  mbali  mpya  za  usalama  barabarani  yawezekana  wakati  wakisoma hazikuwepo ama  zilikuwepo  zimeboreshwa  lakini  pia ubora  wa  miundo  mbinu wa  sasa  ni  tofauti na  wakati  huo .




































Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI