Header Ads Widget

WANANCHI WA KUSINI WAELEZEA WANAVYONUFAIKA NA MRADI WA REGROW




Wakazi wa Kijiji cha Tungamalenga mkoani Iringa wameendelea kutoa shukrani zao kwa Serikali kupitia  Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) jinsi unavyosaidia Wananchi wanaoishi pembezoni mwa Hifadhi za Kipaumbele kwa kutoa ufadhili wa masomo wa vyuo mbalimbali hapa nchini .


Wakizungumza wananchi  hao katika Kijiji cha Tungamalenga kwa nyakati tofauti  wamesema Mradi huo umewanufaisha wananchi hao  kiuchumi na kielimu kwa ustawi wa watoto wao.


Anjelika Kasimba, ambaye ni Mnufaika wa Mradi wa REGROW amesema  REGROW ni  miongoni mwa mradi bora ambao mara baada ya kukamilika kwake utaacha alama isiyofutika kwani anaamini  Mtoto wake aliyepata ufadhili wa  masomo  katika  Chuo cha Mafunzo ya Wanyamapori Pasiansi mara baada ya kuhitimu masomo yake atajikwamua kiuchumi yeye pamoja na familia yake .


Ameongeza kwamba tokea Mradi huo uanze kugusa maisha ya wananchi wa Tungamalenga yeye pamoja na Wanawake wenzake wamepata hamasa ya kufanya kazi kwa bidii ili kuweza kurejesha marejesho na pia kuwa Wanufaika wa miradi mbalimbali ya kiuchumi ikiwemo COCOBA na ufugaji nyuki.



Aneth Kyaulilo ambaye ni Mwezeshaji Jamii wa Mradi  wa Regrow amesema  Mradi huo umeboresha maisha ya wananchi ambapo katika Kijiji cha Tungamalenga  hadi sasa kuna vikundi saba ambavyo vimepewa Mil.48 kwa ajili ya kujiendeleza kiuchumi kupitia Mradi wa REGROW 


Ameeleza kuwa Mradi huo wa REGROW umekuwa msaada mkubwa kwa wananchi na mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa na hii imesaidia vikundi mara baada ya kuundwa vimekuwa vikipewa mafunzo namna ya kuanzisha miradi ya kimkakati kiuchumi



Kwa upande wake Mratibu wa Regrow, Dkt. Aenea Saanya amesema moja ya vigezo vya utekelezaji wa Mradi huo ni kuhakikisha Wananchi wanakuwa wanufaika namba moja katika maeneo yote ambapo Mradi huo unapotekelezwa.


Mradi wa REGROW ulianzishwa mwaka 2017 kwa lengo la kupanua wigo wa mazao ya utalii kijiografia kwa kuendeleza Sekta ya Utalii katika Mikoa ya Kusini. Mradi huo unatekelezwa kupitia fedha za mkopo wa masharti nafuu wa Dola za Marekani Milioni 150 kutoka Benki ya Dunia.


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI