Header Ads Widget

WATU 14 WAMEFARIKI KWA MAFURIKO SOMALIA

 




Watu 14 wameripotiwa kufariki dunia Kusini mwa Somalia baada ya mvua kubwa kunyesha na kusababisha mafuriko, shirika la habari la AFP liliripoti Jumamosi.

 

Pia mvua hizo zilisababisha uharibifu mkubwa katika miji na vijiji kadhaa,

 

Katika mji wa Baardhere jimbo la Jubaland, walifariki watu watatu wa familia moja, mkuu wa wilaya Mohamed Weli, aliwaambia waandishi wa habari alipofanya nao mahojiano.

“Wengi wa majeruhi walinaswa kwenye daraja katika mji ambalo lilisombwa na mafuriko, ilikuwa vigumu sana kuwaokoa watu hawa kwa sababu ya muda tukio lilitokea na ukosefu wa rasilimali katika mji,” alisema Weli.

 

Mvua hizo zinaashiria kuanza mapema kwa msimu wa mvua wa Aprili hadi Juni na zimeleta afueni katika maeneo ya nchi yanayokumbwa na ukame mbaya zaidi katika miongo minne.

 

Lakini shirika la Umoja wa Mataifa la kushughulikia masuala ya kibinadamu OCHA lilionya katika taarifa yake ya Jumamosi juu ya hatari ya kuongezeka kwa magonjwa kama vile kipindupindu, kwani hali ya maisha inaweza kuzorota.

 

Mkazi wa Baardhere, Ahmed Omar alisema kumekuwa na mvua kubwa katika eneo hilo kwa siku tatu mfululizo.

 

“Mafuriko yaliharibu mji wa Baardhere, nyumba yangu iliharibiwa na mali zangu nyingi zilisombwa na mafuriko. Namshukuru Mungu familia yangu ilinusurika, lakini watu watano walikufa katika mtaa wangu wakiwemo watoto na wanawake,” aliiambia AFP.

 

Ahmed aliongeza kuwa kwa sasa mji mzima uko chini ya maji na familia nyingi zilikimbilia maeneo ya juu yaliyoinuka.

 

Kiongozi wa Jubaland, Ahmed Islam alituma salamu za rambirambi kwa ndugu wa waliopoteza maisha na kutaka usaidizi wa haraka upelekwe kwa walioathiriwa na maafa hayo.

 

Pembe ya Afrika ni moja wapo ya maeneo yaliyo hatarini zaidi kwa mabadiliko ya hali ya hewa.

 

Mapema mwezi huu, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilionya kuwa karibu watu 100,000 nchini Somalia wanakabiliwa na viwango vya janga la njaa kutokana na ukame mbaya zaidi kuwahi kukumba eneo hilo katika miongo minne.


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI