NA HADIJA OMARY_LINDI.
JUMLA ya Watoto 166,605 walio chini ya miaka mitano Mkoani Lindi wanatarajiwa kupatiwa chanjo ya Polio (matone) kupitia zoezi la kampeni ya kitaifa la utoaji wa chanjo hiyo inayotarajiwa kufanyika kuanzia April 28 hadi mei 1, 2022 Nchi mzima
Akizungumza Katika kikao cha kamati ya Afya ya msingi Mkoa juu ya kampeni ya kitaifa ya chanjo ya polio Mkuu wa Mkoa wa Lindi Zainab Telack aliwahakikishia wananchi kuwa chanjo hiyo ni salama ambapo imekuwa ikitolewa kwa watoto kwa muda mrefu katika vituo vya kutolea huduma
Hata hivyo Bi. Telack amehimiza wataalam kupeleka elimu kwa wananchi hasa wazazi ili watambue umuhimu wa chanjo hiyo ya polio itakayowakinga watoto wao na ugonjwa huo
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Kheri Kyaga akizungumzia juu ya chanjo hiyo ya polio alisema kuwa lengo la kampeni hiyo ni kuhakikisha wanazuia kuingia kwa ugonjwa huo hapa Nchini ambao umebainika Nchi jirani ya Malawi
Alisema kampeni hiyo itasaidia kuongeza kinga kwa watoto kwa kuwapatia chanjo matone ya polio hata kama wamepata chanjo hiyo awali katika vituo vya kutolea huduma za Afya
" serikali kupitia wizara ya afya na shirika la afya duniani (WHO) wameona ni vyema kuwakinga watoto wote walio chini ya umri wa miaka mitano wasiweze kupata polio na hatua hiyo imefikiwa kutokana na kuwepo kwa mlipuko wa ugonjwa huo katika nchi jirani ya Malawi"
Ameeleza kuwa kampeni hiyo ya chanjo itatolewa kwa kutumia mkakati wa kutembe nyumba kwa nyumba , pamoja na maeneo yenye mikusanyiko ya watu kama vile masoko, shule , misikiti, mashambani , vituo vya mabasi na makambi ya Wavuvi ambapo timu ya wachanjaji katika maeneo hayo kutoa huduma hiyo kwa siku nne.
Nae Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma na Mawasiliano Bi. Habiba Chitanda alisema kuwa ni vyema wazazi wakajitokeza kuwachanja watoto wao kwani ugonjwa huo wa polio hauna tiba zaidi ya chanjo
" Ugonjwa huu wa Polio hautibiki zaidi ya kuzuilika , Mtoto akishapata polio hatoweza kupona tena atapata ulemavu wa kudumu mpaka kifo lakini kama wazazi tutajitokeza kuwachanja watoto wetu waliochini ya umri wa miaka mitano tunaweza kuwanusuru na ugonjwa huo" alisema Bi Chitanda
Nae Fatuma Selemani Mkazi wa Manispaa ya Lindi ameipongeza Serikali kwa kuchukua jitahada haraka za kukabiliana na ugonjwa huo kwa maslahi mapata ya Taifa
0 Comments