Teddy Kilanga, Arusha
Katika kufanikisha utekelezaji wa mpango mkakati wa maboresho wa awamu ya pili wa mwaka 2020/2025,Mahakama ya Tanzania imeazimia kuwashirikisha wananchi kwenye miradi yake kwa lengo la kupanua fikra juu ya utendaji kazi wa muhimili huo baina ya wataalamu na jamii.
Akizungumza wakati wa kufunga kikao kazi cha kujadili mpango mkakati wa Kikao kazi cha mapitio ya mpango mkakati wa pili wa mwaka huo,Mtendaji mkuu wa Mahakama,Prof.Elisante Ole Gabriel alisema mpango huo utakuwa shirikishi kuanzia ngazi ya chini ya wananchi hadi uongozi wa juu wa mahakama.
"Ili kutekeleza mpango mkakati huu lazima kila mmoja awajibike katika kufanya kazi kwa umoja kwa kutambua umuhimu wa bidhaa wanayotoa ikiwa ni pamoja na kujenga tabia ya kutoa mrejesho wa utekelezaji wake,"alisema Prof.Gabriel.
Alisema wakijijengea tabia ya kutoa mrejesho kwa wakati wa utekelezaji mpango mkakati wataendelea kuleta mageuzi makubwa katika muhimili wa mahakama hivyo ni lazima wayaishi yale yote waliyojipangia katika utekelezaji wake.
Aidha alisema wamejipanga kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo ili kuondokana na changamoto zilizojitokeza hapo awali za mpango mkakati wa kwanza ikiwa ni pamoja na ukosefu wa fikra,kutokuwepo umiliki,ukosefu wa ushirikishwaji na ufuatiliaji.
Kwa upande wake Msajili Mkuu wa mahakama ya Tanzania,Wilbert Juma mpango huo ni shirikishi hali ambayo itasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya utoaji wa haki hivyo wanategemea mambo mengi yatahimarika ikiwemo ujio wa mahakama mtandao.
"Kwa hiyo mipango iliyowekwa tunategema yatatekelezwa kwa asilimia kubwa tulizojipangia ikiwa haya yote yanalengo la upatikanaji wa haki kwa umma na tumesisitiza watu washiriki katika programu hii ili kuwa mabalozi wa mpango mkakati huu katika utekelezaji wake,"Alisema Msajili Mkuu.
Vilevile alisema watakuwa mabalozi katika kuhakikisha kwamba ushiriki huo wa uandaji wa mpango kazi wa utekelezaji unawafikia wataalamu wa mahakama ambapo hawakuweza kuhudhuria na kuweza kuuishi mpango huo.
Kwa upande wake,Dkt.Angelo Rumisha alisema lengo ni kufanya uboreshaji wa utoaji wa huduma za mahakama ili kumfikia mwananchi wa chini ambapo maboresho hayo yalianza tangu mwaka 2015 katika mpango mkakati wa kwanza.
"Na katika mpango mkakati huu wa pili uboreshaji ni mkubwa ikiwa ni pamoja na kuanzisha huduma za mahakama kuu katika mikoa yote ya Tanzania hadi kufikia mwaka 2024 lengo hili litakuwa limekamilika kwani iliyopo ni mikoa tisa tu,"alisema Dkt.Rumisha.
Dkt.Rumisha alisema kwa sasa wanatoa huduma zinazomlenga mwananchi kwani upo mpango wa mahakama kufuata wananchi kupitia Mahakama zinazotembea lengo ni kufikisha elimu ya utoaji haki.
0 Comments