Header Ads Widget

KAMATI YA MSHIKAMANO WA TANZANIA NA SAHARA MAGHARIBI YATOA TAMKO

 




Kamati ya Mshikamano wa Tanzania na Sahara Magharibi, inayojumuisha vijana wa 

Kitanzania, inapenda kueleza azma yake ya kuendeleza fikra na misimamo dhahiri na 

ya dhati ya ukombozi wa bara la Afrika, kama ilivyoasisiwa na viongozi na wazee wetu, 

wakiwemo Mwalimu Nyerere na wenzake.

Nchi yetu, tangu kipindi cha kupigania uhuru na kipindi chote baada ya uhuru, 

imechukua jukumu, imejivika wajibu na kuwa mstari wa mbele katika kutetea na 

kusimamia azma ya ukombozi wa bara zima la Afrika.

Kama vijana wa Tanzania na Afrika, tuna kila sababu ya kihistoria na haki ya sheria na 

kisiasa ya kuendeleza harakati na jitihada zote zilizoasisiwa na wazee na viongozi wetu 

katika ukombozi wa bara la Afrika. Hatuna budi kuelewa kwamba ajenda ya ukombozi 

wa bara la Afrika ni urithi wetu, tunapaswa kuienzi na kuiendeleza ajenda hii kwa 

maendeleo ya bara letu.



Leo hii, Kamati ya Mshikamano wa Tanzania na Sahara Magharibi, tunawajibika kueleza 

masikitiko yetu juu ya muenendo wa nchi ya Falme ya Morocco kuendelea kuikalia 

kimabavu Jamhuri ya Kidemokrasia ya Sahara Magharibi.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Sahara Magharibi ni nchi huru iliyopata uhuru wake kutoka 

kwenye utawala dhalimu wa kikoloni wa Hispania; hata hivyo, tangu kupata uhuru wake 

mwaka 1975, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Sahara Magharibi, tofauti na Tanzania na 

nchi nyengine za Afrika, haijapata nafasi na wasaa wa kufurahia uhuru wake, kwani 

tangu mwaka huo Morocco, ikiwa imejawa na hila, ilijitwalia mamlaka na kujimilikisha 

nchi ya Sahara Magharibi; ambapo iliitangaza nchi hiyo ya Sahara Magharibi kuwa ni 

sehemu ya Morocco.



Ni zaidi ya miaka 45 sasa, bado watu wa Sahara Magharibi wanadai uhuru wao kamili 

kutoka kwenye makucha ya ukoloni na kukaliwa kimabavu na nchi ya Falme ya 

Morocco. Sisi kama vijana wa Tanzania, tuna kila sababu ya kuungana na kushikamana 

na watu wa Sahara Magharibi dhidi ya udhalimu wa Morocco.

Miaka ya karibuni, hususani tangu 2017 Morocco waliporudishwa kiholela na kupewa 

uanachama katika Umoja wa Afrika ili hali nchi hiyo inakiuka misingi ya Umoja huo wa 

Afrika, nchi ya Morocco wamekuwa wakieneza propaganda nchini, katika bara la Afrika 

na duniani kwa ujumla dhidi ya Sahara Magharibi.

Kamati ya Mshikamano wa Tanzania na Sahara Magharibi inapinga na kukemea vitendo 

vyote vya udanganyifu vinavyofanywa na vinavyolenga kuupotosha umma na vyombo 

vyake kuhusu hali ya ukombozi wa nchi ya Sahara Magharibi.

Tumeshuhudia wasomi, waandishi, vyombo kadhaa vya habari na hata baadhi ya 

viongozi wakiwa wahanga wa hadaa zinazoeleza kwamba eneo lote la Sahara

Magharibi ni sehemu ya Morocco. Makundi haya ya watu waliohadaika, nayo 

wamegeuka na kuwa vibaraka na vinara katika kueneza na kuendeleza upotoshaji 

kuhusiana na ukombozi wa Sahara Magharibi.

Jitihada hizi, zilizojaa hila, zinaendelea kwa kasi na hata tunatambua kwamba Morocco 

inafanya jitihada ya kukutana na taasisi kadhaa za kiraia na viongozi wake; ambapo 

inatarajia kuzitumia taasisi hizo na viongozi wa taasisi hizo katika kuwatangaza wao 

kama utawala halali wa nchi ya Sahara Magharibi, kwa kuwaeleza kuwa Morocco kama 

ndio suluhu ya kweli na ya kudumu katika kuisaka na kuipata amani na kuyaendea 

maendeleo katika nchi ya Sahara Magharibi.

Tunaeleza kusikitishwa kwetu na makundi yote ya kijamii ambayo yamekumbwa na 

upepo wa laghai za Morocco. Hivyo, kutokana na hali hii tunadhamiria kueleza kwa 

makundi hayo na kwa umma wa Watanzania ya kwamba:

⦁ Sahara Magharibi ni nchi huru iliyopata uhuru mwaka 1975 na Morocco iliivamia 

Sahara Magharibi na kuifanya nchi hiyo kuwa koloni lake tangu wakati huo, kwa 

zaidi ya miaka 45 sasa;

⦁ Sahara Magharibi ni miongoni mwa nchi wanachama zilizounda Umoja wa Afrika 

mwaka 2002 na tangu kuanza kwa Umoja wa Afrika mpaka sasa Sahara 

Magharibi imekuwa ikitambulika kama nchi huru na Umoja wa Afrika (AU);

⦁ Umoja wa Mataifa unatambua eneo zima la Sahara Magharibi kama eneo la 

watu wa Saharawi, watu wa Sahara Magharibi, na eneo hilo sio sehemu ya 

Morocco;

⦁ Katika nyakati tofauti Mahakama ya Umoja wa Ulaya umeendelea kulitambua 

eneo la Sahara Magharibi kuwa ni eneo la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Sahara 

Magharibi na sio eneo la Morocco, na hivyo imebatilisha na kuzuia mikataba 

mbalimbali ya kibiashara iliyoingiwa na nchi za Ulaya na Morocco iliyokuwa 

ikihusianisha rasilimali za Sahara Magharibi, kwa misingi ya kwamba mikataba 

yote inayohusiana na eneo na mali za Sahara Magharibi inapaswa kuingiwa na 

Sahara Magharibi na sio Morocco, kwani ni nchi mbili tofauti.

Tunaeleza ya kwamba, iwapo Morocco ina dhamira ya dhati ya kuendeleza amani na 

kuchangia katika maendeleo ya Sahara Magharibi na bara la Afrika, nao Morocco 

hawana budi kuheshimu maamuzi ya Umoja wa Mataifa yaliyounda MINURSO na 

waruhusu kufanyika kwa uchaguzi wa huru na haki utakao waruhusu watu wa Sahara 

Magharibi kuamua hatma ya eneo lao – ama kujitawala au kuwa chini ya utawala wa 

Morocco.

Kamati ya Mshikamano wa Tanzania na Sahara Magharibi tunatoa wito kwa taasisi za 

kiraia, watetezi wa haki nchini, wasomi, waandishi na vyombo vya habari, wanasiasa, 

taasisi za kiserikali na wananchi kwa ujumla, kuepuka kudanganyika na propaganda za 

Morocco dhidi ya watu wa Sahara Magharibi ambapo Morocco inajaribu kuhalalisha 

udhalimu wanaoufanya kwa watu hao. Hususani, tunatoa wito kwa mashirika, taasisi na 

watu wote kupuuza wito na kutoshiriki semina ya kipropaganda ya Morocco inayolenga 

kueleza kuhusiana na ukuu wa Morocco katika nchi ya Sahara Magharibi.

Ikiwa ni wiki ya kumuenzi Mwalimu Nyerere, Kamati ya Mshikamano wa Tanzania na 

Sahara Magharibi tunaihimiza serikali kuendelea kusimamia msimamo wa nchi wa 

ukombozi wa watu wa Sahara Magharibi na ukombozi wa bara zima la Afrika kama 

ulivyohimizwa na kusimamiwa na Hayati Baba wa Taifa na wenzake.

Vivyo hivyo tunatoa wito kwa Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa kusimama kidete 

na watu wa Sahara Magharibi na kuwanusuru na miaka mengine ya giza, kadhia, 

dhoruba na tabu chini ya utawala wa kikoloni na wa kimabavu wa Morocco katika nchi 

yao.

#TunasimamaNaSaharaMagharibi #TunasimamaNaAfrika

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI