Mama Wajawazito na watoto wanaoishi kambi ya Wakimbizi Nduta wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma na wananchi wa vijiji saba wanaoishi kuzunguka kambi hiyo ya wakimbizi wanatarajia kunufaika na mradi wa afya na kuboresha lishe unaotekelezwa na Shirika la Medical Team International (MTI)
Akizungumza katika uzinduzi wa mradi huo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la MTI, Debora Niyeha alisema kuwa mradi huo mdogo unalenga kuwafikia mama wajawazito na watoto 51,200 kwenye kambi za wakimbizi na vijiji vinavyozunguka kambi hizo kwa ajili ya kutoa huduma za afya kwenye vituo vitatu vinavyozunguka kambi hizo.
Mkurugenzi huyo alisema kuwa katika vituo vyao vya kutoa huduma za afya kwenye kambi za wakimbizi vimeonyesha mafanikio kwa mama wajawazito na watoto kwani tangu mwaka 2020 vituo hivyo vilivyoanza hakuna kifo cha mama mjamzito na mtoto aliyekufa hivyo mpango huo wanataka kuupeleka kwenye vijiji vinavyozunguka kambi za wakimbizi.
Akizindua mradi huo Kaimu Katibu Tawala wa mkoa Kigoma, Elisante Mbwilo alisema kuwa Kupunguzwa kwa kiwango cha chakula kwa asilimia 50 kwenye makambi ya wakimbizi wa Burundi na jamhuri ya kidemokrasi ya Congo Wakimbizi wanaohifadhiwa mkoani Kigoma imesababishwa utapiamlo kwa wakimbizi.
Mbwilo alisema kuwa takwimu hizo zinazotokana na utafiti wa lishe uliofanywa kwenye kambi hizo za wakimbizi mwaka 2023 na kwamba kuzinduliwa kwa mradi huo kutasaidia kukabili utapiamlo hasa kwa mama wajawazito na watoto watakaozaliwa.
Kwa upande wake Mratibu wa Afya wa Shirika la MTI,Dk. Eddah Ndabila alisema kuwa mradi huo uliozinduliwa utatekelezwa wilaya ya Kibondo ambapo msisitizo ni kuhakikisha jamii inajengewe uwezo kuwezesha mama wajawazito kuhudhuria kliniki katika wiki 12 za mwanzo za ujauzito kwani hiyo inasaidia kukabili vifo na changamoto kwa mama wajawazito na watoto.
0 Comments