Header Ads Widget

UNAWEZA KUMEZA 'VIDONGE VYA KINYESI'? HUTIBU BAKTERIA

Madaktari wa Uingereza wamebuni njia mpya ya kusafisha utumbo kukabiliana na vijidudu sugu vinavyojulikana kama "superbugs," wakitumia vidonge vyenye kinyesi kilichokaushwa kwa kugandishwa.

Utafiti huu mpya unalenga wagonjwa ambao wameambukizwa bakteria sugu ndani ya miezi sita iliyopita.

Katika vipimo hivi, kinyesi kinachukuliwa kutoka kwa wachangiaji wenye afya. Kila sampuli ya kinyesi hupimwa ili kuhakikisha haina bakteria hatari, chakula ambacho hakijameng'enywa huondolewa, kisha kinakaushwa kwa kugandishwa na kusagwa kuwa unga.

Unga huo huhifadhiwa kwenye tembe (kidonge) inayoweza kupita tumboni bila kuathirika na kufika kwenye utumbo. Huko, inafunguka na kutoa unga huo kwenye kinyesi.

Huu ni mpango mpya wa kupambana na vijidudu sugu dhidi ya antibiotics na ambavyo huua karibu watu milioni moja kila mwaka.

Kwa mujibu wa Dkt. Blair Merrick, anayeongoza utafiti wa vidonge hivi, utumbo ni "chanzo kikubwa zaidi cha usugu wa viua sumu katika mwili wa binadamu." Vijidudu sugu vya dawa vinaweza kuenea kutoka kwenye utumbo kwenda sehemu nyingine za mwili, kama vile njia ya mkojo au damu, na kusababisha maambukizi.

Wazo la kidonge cha kinyesi si jipya. Upandikizaji wa kinyesi (kuingiza kinyesi kilichosindikwa chenye vijidudu vyenye manufaa kwenye utumbo) hutumika kutibu kuhara kunakosababishwa na bakteria aina ya Clostridium difficile. Tiba hii iliwafanya wanasayansi kugundua kuwa kutumia vijidudu vyenye manufaa kunaweza pia kusaidia kutoa vijidudu vingine hatari kutoka utumboni na kusafisha utumbo.

Jaribio lilifanyika kwa wagonjwa 41 katika hospitali mbili za London, Uingereza ili kufungua njia kwa utafiti mkubwa zaidi.

Sampuli za kinyesi zilipimwa ili kuhakikisha hazikuwa na vitu vyovyote vya hatari.

Dkt. Merrick anasema kuna "dalili zinazotia matumaini makubwa" kwamba vidonge vya kinyesi vinaweza kusaidia kukabiliana na tatizo la vijidudu sugu vya dawa. Bakteria zinazoingizwa tumboni kwa njia hii hushindana kwa chakula na nafasi, na matokeo yake, mwili huweza kuziondoa au "kuzipunguza hadi kufikia hatua ambapo hazisababishi tatizo."

Utafiti huo pia unaonyesha kwamba baada ya matibabu, utofauti wa bakteria tumboni huongezeka. Hii ni ishara ya afya na inaweza kusaidia kuzuia maambukizi mapya kwa kufanya iwe ngumu kwa vijidudu hatari kuingia.

Dkt. Merrick alielezea matokeo hayo kama "ya kufurahisha," akisema: "Haya ni mabadiliko makubwa kutoka miaka 20 iliyopita tulipofikiri bakteria na virusi vyote ni vibaya kwetu, lakini sasa tunagundua kuwa ni muhimu kabisa kwa afya yetu."

Watafiti wanasema kwamba ikiwa vidonge vya kinyesi vitathibitishwa kuwa na ufanisi katika kupambana na vijidudu sugu vya dawa katika tafiti kubwa zaidi, vinaweza kutumika kuzuia na kutibu watu walio katika hatari.

Mapema wiki hii, wanasayansi nchini Uingereza walisema kwamba bakteria wa kwanza tunaokutana nao katika masaa ya kwanza baada ya kuzaliwa wanaweza kutulinda kutokana na maambukizi hatari na inaonekana kupunguza hatari ya watoto wadogo kulazwa hospitalini kwa maambukizi ya mapafu kwa takribani nusu ya ilivyo sasa.

Jumla ya seli zinazounda mwili wa binadamu ni chache kuliko idadi ya bakteria, fangasi, na viumbe wengine vidogo vinavyoishi katika miili yetu (vinavyojulikana kama microbiome). Baadhi ya tafiti zinazohusisha microbiome katika magonjwa mbalimbali, kuanzia ugonjwa wa Crohn (ugonjwa wa kuvimba utumbo) hadi saratani na afya ya akili.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI