Na Matukio Daima Media
Shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu, Amnesty International, limeitaka serikali ya Tanzania kumwachilia mara moja na bila masharti yoyote kiongozi wa chama cha upinzani Chadema, Tundu Lissu, aliyekamatwa na kufunguliwa mashtaka ya uhaini.
Lissu alikamatwa Jumatano akiwa pamoja na wanachama wengine wa Chadema baada ya kuhudhuria mkutano wa hadhara uliofanyika katika mji wa Mbinga, mkoani Ruvuma, kusini mwa Tanzania.
Kwa mujibu wa taarifa ya Chadema, polisi walivamia mkutano huo na kuwatawanya wananchi kwa kutumia mabomu ya machozi.
Kesho yake, Alhamisi, Lissu alipelekwa katika mahakama jijini Dar es Salaam na kufunguliwa mashtaka ya uhaini - kosa ambalo linaweza kupewa adhabu ya kifo.
"Tunaitaka serikali ya Tanzania imwachilie Tundu Lissu mara moja na bila masharti yoyote," alisema Tigere Chagutah, mkurugenzi wa kanda wa Amnesty International kwa Afrika Mashariki na Kusini, katika taarifa yake siku ya Ijumaa jioni.
0 Comments