Na Hamida Ramadhan,Dodoma
JESHI la Kujenga Taifa limetoa onyo kwa wananchi wanaoghushi vyeti vya Mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa ajili ya kujitafutia ajira huku likisema kwa waliobanika na watakaobainika kufanya hivyo kwa matumizi yoyote watachukuliwa hatua kali za kisheria .
Hayo yameelezwa Jijini Dodoma na Kaimu Mkuu wa Tawi la Utawala (JKT) Kanali Juma Mrai wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kujitokeza kwa vitendo vya kughushi vyeti hivyo,amesema vyeti hivyo vinapatikana kwa njia ya kufanya mafunzo na kuhitimu na siyo kughushi.
"Nafasi za kujiunga na Mafunzo ya JKT ,zinatolewa kila mwaka kwa vijana wa kitanzania wenye sifa ,ili wamalizapo Mafunzo ya JKT ,waweze kupata cheti cha kuhitimu Mafunzo ya JKT kihalali,"amesema Kanali Mrai.
Taarifa hiyo ya JKT imekuja kufuatia kubainika kuwepo kwa vyeti vya kughushi vilivyotumika na baadhi ya vijana ambao siyo waaminifu ili kujipatia ajira katika Taasisi na Makampuni yanayohitaji watendaji waliopitia Mafunzo ya JKT.
Amesema ,nafasi za kujiunga na JKT zinatolewa kwa kutangazwa katika vyombo vya habari na mitandao mbalimbali ya kijamii hapa nchini ,hivyo wananchi waepuke kutapeliwa kwa namna yoyote ile ikiwemo kutumiwa ujumbe mfupi wa maneno katika simu zao,kupigiwa simu na kutakiwa kutoa kiasi Fulani change cha fedha ili kupata nafasi hizo.
Ametumia nafasi hiyo kutoa Rai kwa wananchi kwamba,kwa yeyote atakayepokea ujumbe wa namna hiyo atoe taarifa haraka katika kambi yoyote ya Jeshi au kituo chochote Cha polisi kilicho karibu naye.
Aidha Kanali Mrai amesema,JKT lipo tayari kutoa ushirikiano kwa Taasisi na Makampuni yote yanayohitajibuhakikibqa vyeti vya JKT kwa watumishi wao waliopitia Mafunzo ya JKT.
Mwisho
0 Comments