NA WILLIUM PAUL, MOSHI
JESHI la Polisi mkoani Kilimanjaro linawashikilia Askari wawili wa Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro(Kinapa) pamoja na Askari mmoja wa Jeshi la Akiba (Mgambo) kwa tuhuma za mauaji ya Octavian Temba(39) mkazi kijiji cha Komela kata ya Marangu magharibi wilayani Moshi.
Akielezea tukio hilo Mwenyekiti wa Ulinzi na usalama na Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu alisema kuwa, Mei 9 mwaka huu kulitokea purukushani kati ya Askari wa Kinapa pamoja na mwananchi aliyekuwa akikata majani pembezoni mwa eneo la hifadhi na kupigwa risasi.
“Katika purukushane hizo kulitokea bahati mbaya akapigwa risasi na kupoteza maisha, Jeshi la la polisi limewatia mbaroni Askari wa Uhifadhi wawili, pamoja na jeshi la Akiba (Mgambo) kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Ila niwaombe wananchi ikiwa tukio limetokea na tayari wamechukuliwa hatua, sio vyema kuchukua sheria mkononi.Jana kuna wananchi zaidi 200 walifanya maandamano yasiyo rasmi mpaka kwenye geti la Kinapa,wakafanya vurugu, wameharibu miundombinu, Wamekata barabara ambayo imejengwa kwa gharama kubwa, wamekata mabomba ya maji, na kusababisha baadhi ya wageni kuchukua muda mrefu kutokana na hofu iliyotanda kufuatia maandamano,” alisema
0 Comments